Kukamatwa kwa Mamia ya Waandamanaji wa Amani Wanaounga Mkono Palestina Nchini Uingereza
Ni Ushahidi wa Uigizaji wa Demokrasia
(Imetafsiriwa)
Habari:
Siku ya Jumamosi, Septemba 6, karibu watu 900 walikamatwa katika maandamano ya kuunga mkono Palestina huko London, walipokuwa wakiandamana dhidi ya mauaji ya halaiki yanayoendelea na njaa ya watu wa Gaza, pamoja na kupigwa marufuku kwa kundi la "Palestina Action" ambalo serikali ya Uingereza ililitaja kama shirika la kigaidi mwezi Julai. Miongoni mwa waliokamatwa walikuwa mapadri, wachungaji, walimu, madaktari, wafanyakazi wengine wa afya na watoto wa manusura wa Holocaust pamoja na waandamanaji wenye ulemavu. Wengi wao walikuwa wazee - katika miaka ya sitini, sabini na hata themanini - akiwemo mtu kipofu mwenye umri wa miaka 62 kwenye kiti cha magurudumu. Polisi waliwapeleka mamia ya waandamanaji wa amani kwa sababu tu ya kubeba bango lililoandikwa "Ninapinga mauaji ya kimbari. Ninaunga mkono Palestina Action". Zaidi ya watu 700 walikuwa wamekamatwa katika maandamano kama hayo ya awali dhidi ya mauaji ya kimbari yanayoendelea huko Gaza kwa kuunga mkono shirika hili.
Maoni:
Palestina Action ni shirika lenye makao yake makuu nchini Uingereza, na limetangaza kwamba lengo lake ni "kukomesha ushiriki wa kimataifa katika mfumo wa mauaji ya kimbari na ubaguzi wa rangi wa Israel", kama vile kusimamisha usambazaji wa silaha kutoka Uingereza kwenda kwa taasisi ya Kiyahudi, ambayo inajumuisha kukwamisha shughuli za viwanda vya silaha vinavyohusiana nayo, kwa mfano, tawi la Uingereza la Elbit Systems, kampuni kubwa zaidi ya Kizayuni inayotengeneza silaha. Baadhi ya wanachama wa shirika hili wamechukua hatua za moja kwa moja katika jaribio la kufikia malengo yao, ikiwa ni pamoja na kuvamia kambi ya ndege ya Jeshi la Wanahewa la Kifalme la Uingereza la Brize Norton mwezi Juni na kuharibu ndege mbili za Voyager, ambazo shirika hilo lilisema zilikuwa maandamano dhidi ya mauzo ya serikali ya silaha kwa uvamizi. Imeripotiwa kuwa kambi hiyo ya ndege ilitumiwa na ndege za kivita zinazomilikiwa na taasisi ya Kiyahudi zilizoshiriki katika kulipua Gaza. Shirika hili liliwekwa kama shirika la kigaidi muda mfupi baada ya tukio hili, na kufanya uanachama au kuonyesha msaada wa umma kwake kuwa uhalifu unaoadhibiwa na kifungo cha hadi miaka 14 jela.
Baada ya marufuku hii, mamia ya waandamanaji walikamatwa chini ya sheria ya ugaidi katika maandamano ya amani yanayounga mkono Palestina, kwa sababu tu ya kuonyesha msaada wowote au uhusiano na shirika hilo. Mnamo Mei 2024, ukaguzi wa serikali, ambao ulidaiwa kuwa huru, ulinganisha vurugu za kisiasa na machafuko yanayosababishwa na vuguvugu la Palestina Action na "makundi ya kigaidi", na ilipendekeza kupiga marufuku shughuli zake. Inashangaza kwamba mwandishi wa ukaguzi huo, John Woodcock, alikuwa mshauri anayelipwa wa makundi ya ushawishi anayowakilisha watengenezaji silaha, pamoja na kuwa Mwenyekiti wa zamani wa kundi la "Marafiki wa Israel" katika Chama cha Leba.
Ukweli kwamba serikali ya Uingereza haioni aibu kukamata mamia ya waandamanaji wa amani ambao wanaandamana dhidi ya mauaji ya halaiki na njaa ya watu huko Gaza, huku ikiwa inashiriki katika mauaji haya kwa kuruhusu utengenezaji na uuzaji wa silaha kusaidia katika hilo, unaonyesha kikamilifu utupu wa kimaadili na ukosefu wa ubinadamu katika mfumo wake wa kidemokrasia. Mashirika mengine huko nyuma yamechukua hatua za moja kwa moja kwa ajili ya madai yao, ikiwa ni pamoja na utetezi wa haki ya wanawake kupiga kura, wanaharakati wa hali ya hewa, na makundi ya haki za wanyama, hata hivyo, ukweli kwamba sheria za ugaidi zinatumiwa dhidi ya mashirika ambayo yanaunga mkono ukombozi wa Palestina, unathibitisha kwamba marufuku hii inalenga waziwazi kuwanyamazisha wale wanaopinga uvamizi na ushirikiano wa serikali ya Uingereza katika mauaji haya ya kimbari. Kerry Moscogiuri wa Amnesty International nchini Uingereza alisema "Wakati serikali inawakamata watu chini ya sheria za ugaidi kwa sababu tu ya kuandamana kwa amani, kuna kitu kibaya sana kinatokea hapa Uingereza".
Mbali na kukamatwa na kuwekwa kizuizini kwa waandamanaji wa amani wanaounga mkono Palestina, maprofesa wa vyuo vikuu, madaktari na wataalamu wengine nchini Uingereza wamenyimwa kazi zao, na wanafunzi wamelazimika kuacha masomo yao kwa kukosoa uvamizi na kuunga mkono ukombozi wa Palestina. Dhuluma hii imesikika katika nchi nyingine za kidemokrasia, ikiwa ni pamoja na Amerika na Ujerumani.
Haya yote yanaonyesha udanganyifu wa uhuru wa kujieleza katika nchi hizi za kidemokrasia ambazo zinakuza ulimwengu na kutoa mihadhara juu ya ubora wa maadili yao ya kiliberali, lakini kwa kweli ziko tayari kuyakandamiza maadili haya na kuyaacha wakati maslahi yao ya kisiasa na kiuchumi yanatishiwa; Kwa sababu faida za kisiasa na kifedha, chini ya mfumo wa kibepari wa kidemokrasia, daima huzidi masuala mengine yote, ikiwa ni pamoja na kulinda utakatifu wa maisha ya binadamu. Ni wazi kwamba maadili na imani za demokrasia zinaweza kubadilika na kugeuzwa, kama vile dhamiri ya kimaadili ya serikali zinazoiongoza! Mfumo wa kidemokrasia unadanganya watu kwamba mamlaka yametolewa kwao, wakati kwa kweli, yamewekwa kwa nguvu mikononi mwa wasomi watawala au matajiri ambao wanatunga sheria na sera kulingana na maslahi yao ya kibinafsi; kisiasa na kiuchumi. Hata uhuru wa kujieleza hupewa na kunyang'anywa watu kulingana na kile kinachofaa serikali kisiasa wakati huo. Zaidi ya hayo, uwajibikaji wa kweli wa watawala ni ndoto tu; ambapo wale wanaohusika na silaha za uvamizi wa mauaji ya kimbari wanaweza kuepuka matokeo yoyote ya kisiasa au kisheria!
Haya yote yanapaswa kuwa somo la wazi kwetu sisi Waislamu, kwamba mfumo wa kidemokrasia, haijalishi una sura gani, hauwezi kamwe kuhakikisha haki kwa watu, wala hauna nguzo ya kimaadili ya kusimamisha mauaji ya kimbari. Utoaji wa haki hautarajiwi na unabadilika, na kuna mstari mwembamba kati ya demokrasia na udikteta, kama inavyoonekana hivi sasa huko Amerika, na katika nchi nyingine nyingi za kidemokrasia. Kukomesha mauaji ya kimbari huko Gaza na kuondoa uvamizi kunahitaji kuanzishwa kwa dola ambayo inajali kweli maisha ya mwanadamu, inatetea ubinadamu na kupinga dhuluma na ukandamizaji wa kila aina, bila kujali matokeo ya kifedha yanayotokana na hilo. Inahitaji dola ambayo ni mlinzi wa Uislamu na Waislamu, na inatumia jeshi lake kutetea madai yake. Dola hii ni Khilafah kwa njia ya Utume ambayo inatawala kwa mujibu wa Qur'an na Sunnah tu. Kwa hivyo, ikiwa tunataka kuona mwisho wa mauaji ambayo umma wetu unakabiliwa nayo huko Palestina, Kashmir, Sudan, Yemen na kwingineko, tunahitaji kufanya kazi mara moja kuanzisha Khilafah, ikiwa ni pamoja na kuzihimiza jeshi za Waislamu kutoa nusra kwa ajili ya kuanzishwa kwake bila kuchelewa.
﴿وَالَّذِينَ كَفَرُوا أَعْمَالُهُمْ كَسَرَابٍ بِقِيعَةٍ يَحْسَبُهُ الظَّمْآنُ مَاء حَتَّى إِذَا جَاءهُ لَمْ يَجِدْهُ شَيْئاً﴾
Imeandikwa kwa ajili ya Radio ya Ofisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir
Asmaa Siddiq