Vyombo vya Ujasusi vya Tajik Vinarudisha Wanafunzi 4000 kutoka Nchi za Nje
(Imetafsiriwa)
Habari:
Mamlaka za Tajikistan zimewarudisha zaidi ya wanafunzi 4000 kutoka nchi za nje kwa kisingizio cha kuzuia uwezekano wa kujiunga kwao na mashirika ya kigaidi. Hii ilitangazwa na Mkuu wa Kamati ya Usalama wa Kitaifa, Saymon Yatimov, wakati wa mkutano uliofanyika Dushanbe. Kulingana naye, vijana hawa walikuwa wakisoma nje ya nchi na walikuwa chini ya ushawishi wa kiitikadi kutoka kwa vikundi vyenye msimamo mkali na taasisi za kidini za elimu ambazo shughuli zao zimezua wasiwasi kwa vyombo vya usalama vya Tajik. Yatimov alisisitiza kwa kusema: "Ili kuzuia kujiunga kwao na vikundi kama hivyo, zaidi ya wanafunzi 4000 wa Tajik wamerejeshwa nchini kwao, ambako walikuwa wanalengwa na mashirika ya kigaidi na taasisi za kigeni za elimu ya kidini."
Maoni:
Ikumbukwe kwamba serikali ya Tajik imekuwa ikiweka udhibiti mkali juu ya elimu ya kidini ya vijana wa Tajik kwa miaka 15. Kila kitu kilianza wakati mwaka wa 2009 ulitangazwa kuwa "Mwaka wa Imam Abu Hanifa". Kwa kisingizio cha kuhifadhi madhehebu ya Hanafi, hatua za ukandamizaji zilichukuliwa dhidi ya wanafunzi wa vyuo vikuu vya kidini, haswa wale wanaosoma nje ya nchi. Katika kipindi cha miaka michache, taasisi zote za elimu ya kidini zilifungwa nchini, isipokuwa Taasisi ya Kiislamu huko Dushanbe, ambayo iko chini ya usimamizi mkali wa serikali.
Tangu wakati huo, kupata elimu ya kidini nchini Tajikistan kumeruhusiwa tu katika taasisi zinazotambuliwa rasmi na kwa idhini ya wazazi. Taasisi pekee inayofanya kazi ya aina hii ni Taasisi ya Kiislamu huko Dushanbe, ambayo inakubali idadi ndogo sana ya wanafunzi. Kama matokeo, kuna uhaba mkubwa wa wataalamu waliohitimu katika uwanja huu. Wengi wa watu wa kidini huru na watu ambao wamepokea elimu ya kidini, wameondoka nchini kwa muda mrefu au wanatumikia vifungo vya jela kwa mashtaka ya jinai yaliyotungwa. Waliobaki wako chini ya uangalizi mkali kutoka kwa vyombo vya usalama.
Moja ya nguzo kuu za sera ya ndani ya Rais Rahmon ni kuzuia aina yoyote ya ufufuo wa kidini na kisiasa, sawa na kile kilichotokea katika miaka ya tisini ya karne iliyopita. Kwa kuzingatia mwelekeo wa sasa, haionekani kuwa chochote katika suala hili kitabadilika hata baada ya kustaafu kwa Rahmon kunakotarajiwa, kwa kuzingatia matamshi yaliyotolewa na mrithi wake. Ni muhimu kuzingatia kwamba mnamo Agosti mwaka huu, Rustam Imam Ali, meya wa Dushanbe na Spika wa Baraza la Wawakilishi, wakati wa mkutano na wawakilishi wa vyombo vya kutekeleza sheria na vyombo vya mahakama katika mji mkuu, alielezea wasiwasi wake juu ya suala la elimu haramu ya kidini. Alisema wakati huo: "Asilimia themanini ya wale ambao wamepokea mafunzo haramu ya kidini ni vijana chini ya umri wa miaka thelathini."
Imeandikwa kwa Idhaa ya Afisi ya Habari Kuu ya Hizb ut-Tahrir
Muhammad Mansour