Umma Unahitaji Khilafah Kulinda Maeneo Yake Matakatifu, Siyo Mkataba wa Ulinzi Kulinda Watawala Vibaraka!
Habari:
Pakistan na Saudi Arabia zimeingia katika mkataba muhimu wa ulinzi wa pamoja, ambapo uchokozi wowote dhidi ya nchi mojawapo utachukuliwa kuwa uchokozi dhidi ya nyingine, na Waziri Mkuu wa Pakistan Shehbaz Sharif na Mwanamfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman walitia saini mkataba wa pamoja wa ulinzi wa kimkakati katika Ikulu ya Al-Yamama huko Riyadh siku ya Jumatano, Septemba 17, 2025. (Chanzo)
Maoni:
Kufuatia shambulio la chuki la Kiyahudi dhidi ya Qatar mnamo Septemba 9, 2025, ambalo liliwalenga viongozi wakuu wa kisiasa wa Hamas, makubaliano haya ya ulinzi yanatangazwa kama majibu yake. Na wazungumzaji wa utawala nchini Pakistan wanauelezea kama mafanikio na ushindi kwa sera ya kigeni ya Pakistan! Hata watawala wanadai kuwa wameheshimiwa kwa kukabidhiwa jukumu la kulinda misikiti mitakatifu huko Makkah na Madina!
Lakini ukweli ni kwamba makubaliano haya si mapya, uhusiano wa kijeshi kati ya Pakistan na Saudi Arabia ulianza mwaka 1967, na uliimarika zaidi baada ya tukio la Al-Juhaymani katika Msikiti Mkuu wa Makkah mwaka 1979 wakati vikosi maalum vya Pakistani vilisaidia kurejesha Msikiti Mtakatifu. Kufikia mwaka 1982, uhusiano huu uliwekwa katika mfumo rasmi kupitia makubaliano ya ushirikiano wa usalama wa pande mbili, ambayo yaliruhusu mafunzo na ushauri kwa vikosi vya Saudi Arabia, na hata kupelekwa kwa makumi ya maelfu ya askari wa Pakistani katika ardhi ya Saudi Arabia. Saudi Arabia pia imekuwa mtoaji mkuu wa silaha za Pakistani, na mwaka 2015, Saudi Arabia ilitangaza kile kinachoitwa "Muungano wa Kijeshi wa Kiislamu wa Kupambana na Ugaidi", na mkuu wa zamani wa majeshi ya Pakistani, Raheel Sharif, aliteuliwa kuwa kamanda wake wa kwanza, lakini, licha ya kelele zote za vyombo vya habari, muungano huu haujawahi kutumiwa kukabiliana na ugaidi wa chuki wa Kiyahudi dhidi ya Waislamu huko Palestina! Hata baada ya shambulio dhidi ya Qatar, jukumu lake halikuamilishwa isipokuwa katika mfumo wa mazoezi ya kijuujuu.
Ama furaha ya serikali ya Pakistani kwa fursa iliyopewa ya kulinda misikiti miwili takatifu, inazua swali: Kwa nini hawaonyeshi shauku sawa ya kukomboa ya tatu; Msikiti wa Al-Aqsa, ambao unakaliwa na Wayahudi tangu 1967, na jeuri zao zinaendelea kuuchafua kila siku?!
Tangu Oktoba 7, 2023, Waislamu nchini Pakistan wanadai jeshi lao lichukue hatua kuisaidia Gaza, kukomboa Msikiti wa Al-Aqsa, na kuufuta uhasama wa Kiyahudi. Hata hivyo, madai haya daima yanakataliwa kwa kisingizio cha hali mbaya ya ndani huko Khyber Pakhtunkhwa na Balochistan, au kutokana na tishio la India. Hata hivyo, uasi katika maeneo hayo haujapungua, wala tishio la India halijapungua, bali India inasubiri fursa ya kuzindua tena "Operesheni Sundar" dhidi ya Pakistan. Kwa hivyo ni wazi kuwa tatizo si uwezo wa kupigana kwenye pande nyingi, bali kile ambacho Marekani inaamuru. Mkataba huu mpya unatumikia maslahi ya Marekani, na haifikiriwi kwamba uongozi vibaraka nchini Pakistan na Saudi Arabia ungechukua uamuzi huo wa kimkakati kwa kujitegemea.
Mawazo kama vile "NATO ya Kiislamu" ni majaribio tu ya kunyonya hasira ya umma kutokana na kushindwa kwa watawala kusaidia Gaza, kwani makubaliano ya ulinzi yanatumikia tu viti vyao vya enzi, na si maeneo matakatifu ya umma, na watawala hawa wanaungana kulinda mifumo yao, lakini hawaungani kukomboa Palestina, na makubaliano haya hayatawahi kuamilishwa dhidi ya muungano wa Marekani na Wayahudi. Umoja wa Waislamu hauwezi kujengwa juu ya misingi ya ulinzi wa pamoja au miungano dhaifu ya kisiasa, bali juu ya itikadi ya Kiislamu pekee. Na wokovu wa umma uko katika kuanzisha Khilafah kwa misingi ya Utume, inayoongozwa na Khalifa anayeziunganisha chini ya bendera ya Tauhidi. Na chochote zaidi ya hicho - iwe ni Shirika la Ushirikiano wa Kiislamu, au Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, au makubaliano ya ulinzi wa pamoja - si lolote ila udanganyifu.
﴿Hakika huu ni umma wenu, umma mmoja, na Mimi ndiye Mola wenu, basi niabuduni﴾
Imeandikwa kwa ajili ya Idhaa ya Ofisi Kuu ya Habari ya Hizb ut-Tahrir
Shahzad Sheikh - Jimbo la Pakistan