Mkataba wa Kibiashara: Udhihirisho wa Utegemezi wa Kiuchumi wa Indonesia kwa Marekani
Habari:
Rais wa Amerika Trump alitangaza mkataba wa kibiashara na Indonesia, ambapo ushuru wa bidhaa za Indonesia ulipunguzwa kutoka 32% hadi 19% baada ya kutishiwa kupanda. Kwa upande mwingine, Indonesia ilikubali kununua nishati ya Amerika yenye thamani ya dola bilioni 15, na bidhaa za kilimo zenye thamani ya dola bilioni 4.5, pamoja na ndege 50 za Boeing, pamoja na ndege za aina ya 777. Trump alitangaza kuwa Amerika itapata ufikiaji kamili wa soko la Indonesia bila kulipa ushuru. Mkataba huo ulifikiwa baada ya mazungumzo na Rais wa Indonesia Prabowo Subianto, lakini tarehe ya kuanza utekelezaji wa kupunguzwa kwa ushuru na ununuzi haijaamuliwa bado. Kiasi cha biashara kati ya Indonesia na Amerika kilifikia karibu dola bilioni 40 mwaka 2024, na nakisi ya biashara ya Amerika ilifikia karibu dola bilioni 18. Mkataba huu unakuja kama sehemu ya juhudi za Trump za kufanya makubaliano kama hayo ya kibiashara na nchi kama vile Uingereza, Vietnam na China, huku mazungumzo yakiendelea na India na Umoja wa Ulaya, ili kushughulikia kile anachokiona kama vitendo vya kibiashara visivyo vya haki vinavyodhuru maslahi ya Amerika. (The Guardian)
Maoni:
Maendeleo ya hivi karibuni katika uhusiano wa kibiashara kati ya Indonesia na Amerika, ambayo Indonesia imeikaribisha kama mafanikio ya kidiplomasia kwa sababu ya kupunguzwa kwa ushuru wa Amerika kutoka 32% hadi 19%, inaangazia udhaifu wa kimuundo zaidi katika diplomasia ya kimataifa ya Indonesia. Mafanikio haya yanayodaiwa hupoteza umuhimu wake mbele ya ukweli kwamba Amerika imepata makubaliano makubwa; kuingia kamili na bila malipo ya ushuru katika soko la Indonesia, na kulazimisha Indonesia kununua ndege 50 za Boeing, na mikataba ya mabilioni ya dola ya kununua nishati na bidhaa za kilimo za Amerika. Kimsingi, Indonesia haiingii katika mazungumzo ya usawa na yenye mamlaka, lakini inalazimishwa kutii chini ya shinikizo.
Mwenendo huu si mpya. Tangu (uhuru) wa Indonesia, Marekani imecheza jukumu kubwa katika kuunda mwelekeo wa kisiasa na kiuchumi. Kupitia zana kama vile madeni ya nje na utegemezi wa wafadhili, Amerika imeweza kupenya katika michakato ya kufanya maamuzi nchini Indonesia, ikiathiri kila kitu; kutoka ukombozi wa uchumi hadi mtindo wa utawala wa kisiasa. Rasilimali asilia za Indonesia - kutoka mafuta na gesi hadi shaba na dhahabu - zimekuwa zikinyonywa kwa muda mrefu chini ya makubaliano ambayo yana upendeleo usio sawa kwa makampuni ya kigeni, hasa yale yanayohusiana na maslahi ya Amerika.
Kinachotia wasiwasi haswa ni sauti ya sherehe kutoka kwa maafisa wa Indonesia kuhusu kile ambacho kwa kweli ni kulazimishwa kiuchumi! Badala ya kupinga asili isiyo sawa ya makubaliano au kutetea haki ya nchi kulinda viwanda vyake vya kitaifa na uhuru wake wa kiuchumi, serikali imechagua kuwasilisha makubaliano hayo kama mafanikio. Hii inaonyesha mtindo mpana zaidi katika nchi zenye Waislamu wengi, ambapo utegemezi wa baada ya ukoloni na ukosefu wa uhuru wa kweli wa kisiasa unaendelea kuzuia juhudi za kujenga uchumi imara na unaojitosheleza.
Kwa upana zaidi, tukio hili linaangazia udhaifu wa kijiografia wa nchi za Kiislamu. Licha ya kuwa na rasilimali kubwa za asili na watu, bado zinabaki zimegawanyika, dhaifu na haziwezi kujidhihirisha katika ulimwengu. Udhaifu huu sio tu wa kiuchumi, lakini pia wa kisiasa na wa kimsingi. Hii inaeleza kushindwa kwa mara kwa mara kwa nchi zenye Waislamu wengi kuwalinda watu wao, pamoja na kuonyesha mshikamano wa kweli na ndugu zao wanaodhulumiwa, kama vile Wapalestina.
Isipokuwa nchi za Kiislamu zitakapounda mifumo ya kisiasa ambayo inakuza uhuru, umoja na kujitegemea badala ya kujisalimisha kwa nguvu za kigeni na taasisi za kineoliberali, zitaendelea kuwa vyombo tu mikononi mwa nguvu za kimataifa. Uhuru wa kweli unahitaji zaidi ya kupunguza ushuru, unahitaji ujasiri wa kukabiliana na unyonyaji wa kiuchumi na kujenga mfumo ambao unatumikia watu, sio maslahi ya nje.
Imeandikwa kwa Radio ya Ofisi Kuu ya Habari ya Hizb ut-Tahrir
Abdullah Aswar