2025-09-17
Gazeti la Ar-Raya: Mkutano wa Shirika la Ushirikiano la Shanghai
na Ushawishi wa China
Kuanzia Agosti 31 hadi Septemba 1, zaidi ya viongozi ishirini walikutana katika mji wa Tianjin kaskazini mwa China kuhudhuria mkutano wa mara kwa mara wa Shirika la Ushirikiano la Shanghai. Shirika hilo linajumuisha wanachama kumi kamili, pamoja na nchi mbili kama waangalizi, na nchi kumi na nne washirika.
Wakati wa mkutano huo, ilidhihirika wazi kuwa msimamo wa Urusi ndani ya shirika - ambao hapo awali ulikuwa unaonyesha vichwa viwili - umedhoofika, wakati ushawishi wa China uliongezeka sana. Mwishoni mwa mkutano huo, Azimio la Tianjin liliidhinishwa, ambalo lilitaja kutambua haki ya nchi kusimamia mtandao ndani ya ardhi yao, kupanua ushirikiano wa kupambana na ulanguzi wa dawa za kulevya, na makubaliano ya kuanzisha benki moja ya umoja wa shirika.
Baada ya mkutano huo, onyesho la kijeshi lilifanyika mnamo Septemba 3 katika Uwanja wa Tiananmen katikati mwa Beijing na ushiriki wa viongozi hao hao, kuashiria mwisho wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Rais wa Marekani Trump alielezea tukio hili kama njama dhidi ya nchi yake.
Kama inavyojulikana, Shirika la Ushirikiano la Shanghai limechukua jukumu la kukabiliana na changamoto nne kuu: ugaidi, itikadi kali, kujitenga, na ulanguzi wa dawa za kulevya, ili kufikia utulivu na usalama. Hata hivyo, hali halisi inaonyesha kuwa Waislamu ndio wanaobeba mzigo wa makabiliano haya; shirika linapigana na Uislamu, makundi ya Kiislamu na Waislamu chini ya kivuli cha "kupambana na ugaidi na itikadi kali", likijaribu kuweka vizuizi mbele ya juhudi za umma kuanzisha dola ya Khilafa. Pia, Waislamu wanabeba mzigo wa kile kinachoitwa "kupambana na kujitenga", kwani Waislamu katika Caucasus ndani ya Urusi, na Uyghur nchini China, wamekuwa wahasiriwa wa kisingizio hiki.
China:
China inachukuliwa kuwa mmoja wa waanzilishi mashuhuri wa Shirika la Ushirikiano la Shanghai mnamo 2001. Kupitia hiyo, ilifungua mlango kwa upanuzi wake wa kihistoria kuelekea Asia ya Kati. Ukuaji endelevu wa uchumi wa China, dhidi ya kupungua kwa ushawishi wa Urusi katika uwanja wa kimataifa, umempa fursa ya kutekeleza miradi mikubwa katika eneo hilo. Hivyo, mwelekeo wa kiuchumi wa shirika - ambao kimsingi ulilenga usalama wa kikanda - umeanza kuongezeka. Hii inathibitishwa na mpango wa China, ambao umekuwa ukiwasilishwa kwa miaka mingi kuanzisha benki ya maendeleo inayohusiana na shirika, ulipata msaada katika mkutano wa Septemba 1.
Nchi wanachama zimesisitiza umuhimu wa kuanzisha benki ya maendeleo, na zimechukua uamuzi wa kupanga kazi yake na kutoa kila kitu kinachohitajika kufadhili shughuli zake na kuhakikisha uendeshaji wake. Mbali na hayo, China inakusudia kutekeleza miradi midogo mia moja kwa faida ya nchi wanachama wahitaji ndani ya shirika. Kwa madhumuni haya, China itatoa mwaka huu karibu yuan bilioni mbili (takriban dola milioni 280) kama mchango, pamoja na kutoa yuan bilioni kumi kama mikopo.
Rais wa China Xi Jinping hakuzuia kwa hilo, bali alizindua katika hotuba yake wakati wa mkutano matamko dhidi ya "utawala mmoja" na "akili ya Vita Baridi", akilenga Marekani kwa kufanya hivyo.
Pia, mradi wa ukanda mmoja njia moja, umeanza kufungua njia mpya za kuimarisha uhusiano katika uwanja wa usafiri. Kwa mfano, ujenzi wa reli ya China - Kyrgyzstan - Uzbekistan umeanza, na kivuko cha ziada cha mpaka kinafunguliwa kati ya Kyrgyzstan na China kwa jina la Bedel. Kutoka kwa hili, inakuwa wazi kwamba Shirika la Ushirikiano la Shanghai limekuwa chombo mikononi mwa China kuendeleza upanuzi wake wa kiuchumi kuelekea Asia ya Kati, na kisha kwenda Asia ya Kusini.
Urusi:
Urusi pia ni miongoni mwa nchi zilizounda shirika, na lengo lake kuu lilikuwa kuzuia kupenya kwa ushawishi wa Magharibi katika Asia ya Kati. Hata hivyo, kupungua kwa uchumi wa Urusi na hadhi ya kimataifa ya Urusi kulitoa nafasi kwa ukuaji wa ushawishi wa China katika eneo hilo. Mwanzoni, Urusi ilisimama - hata kwa njia isiyo ya moja kwa moja - dhidi ya kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi ndani ya shirika kwa hofu ya ukuaji wa ushawishi wa Kichina kiuchumi katika Asia ya Kati, lakini vita nchini Ukraine iliilazimisha kubadilisha msimamo huu.
Leo, Urusi inaunga mkono msimamo wa China katika uwanja wa kimataifa. Hii inaonekana katika taarifa ya rais wake Putin kuunga mkono mpango uliowasilishwa na Xi Jinping kuhusu utawala wa kimataifa, kwani alisema: "Tumesikiliza kwa makini mapendekezo ya Bw. Xi Jinping kuhusu kujenga mfumo mpya wa kimataifa, wenye ufanisi na vitendo kwa utawala. Mpango huu ni muhimu sana katika hali ya sasa, ambapo baadhi ya nchi bado zinatafuta kulazimisha utawala wao katika mahusiano ya kimataifa. Urusi inaunga mkono mpango wa Rais Xi Jinping, na tunavutiwa na kujadili mapendekezo yaliyotolewa na marafiki zetu wa Kichina." (Sputnik, 2025/9/1)... Kwa hiyo, kupungua kwa jukumu la Urusi ndani ya Shirika la Ushirikiano la Shanghai ni jambo lisilo na ubishi.
India:
Inaweza kuonekana kutoka kwa mtazamo wa nje kwamba Marekani kuweka ushuru wa forodha kwa India kumeisukuma kuelekea ushirikiano na Mashariki. Mbali na hilo, Rais wa Marekani Trump alitoa wito kwa India kupunguza ununuzi wake wa mafuta ya Urusi. Ingawa sehemu ya Urusi katika uagizaji wa mafuta wa India haukuzidi 1% hadi 2022, sasa imeongezeka hadi 42%.
Lakini kwa kweli, licha ya mazungumzo juu ya ushirikiano kati ya India na China, ushindani kati yao ni wazi. Sababu kuu ni kwamba India inafuata sera inayotegemea Magharibi. Pia, mradi wa Njia ya India - Mashariki ya Kati - Ulaya, ulizinduliwa kuwa mbadala shindani kwa mradi wa Ukanda na Njia wa China. Sambamba na hayo, makampuni makubwa ya Marekani yameanza kuhamisha uzalishaji wao wa viwandani kutoka China kwenda India.
Miongoni mwa maonyesho ya misimamo ya kupingana ya India ndani ya shirika ni kwamba ilikataa kujiunga na taarifa iliyotolewa na mkutano wa mawaziri wa ulinzi wa nchi wanachama mnamo Juni, ambayo ililaani mashambulizi ya chombo cha Kiyahudi dhidi ya Iran. India ilieleza msimamo wake kwamba taarifa hiyo ilipuuza matukio ya umwagaji damu yaliyotokea mnamo Aprili 22 na Pakistan; kwa hiyo, msimamo wa India unazidisha migongano na mizozo ndani ya shirika.
Asia ya Kati:
Inaweza kusemwa kuwa nchi za Asia ya Kati zinashiriki katika shirika hili kwa lazima; mahusiano yao ya kimsingi ya kibiashara yanaunganishwa na China na Urusi, na wakati huo huo bado ziko chini ya ushawishi wa Urusi kama mrithi wa Umoja wa Sovieti. Shirika limefanya kazi kuimarisha mahusiano ya nchi hizi na China.
Hata hivyo, nchi hizi zinajaribu kufuata sera ya mwelekeo mwingi. Nchini Kazakhstan na Uzbekistan hasa, uwekezaji mkubwa wa Magharibi unazuia kuchukua msimamo wa nje ambao ni chuki kwa Magharibi. Kyrgyzstan inasimama katika hali tofauti kidogo, kwani inataka kuimarisha uhusiano wake na China na kupata mikopo na misaada kutoka kwake, na kwa hivyo inachukua msimamo dhidi ya Magharibi.
Mbali na hilo, Kyrgyzstan inatoa mfululizo wa mapendekezo ya kuendeleza shirika, hasa ili kuimarisha msimamo wa China ndani yake. Kwa mfano, wakati wa mkutano wa mwisho, mapendekezo yalitolewa ya kujenga njia mpya za usafiri na kuchukua faida ya uwezekano (wa kuvuka - usafiri) wa nchi za shirika, ambayo hutumikia mradi wa Ukanda na Njia. Pia ilitoa wito wa kuharakisha uanzishwaji wa mfumo mzuri wa kifedha kwa shirika, ambao unajumuisha kuanzisha benki ya maendeleo, mfuko wa maendeleo na mwingine wa uwekezaji, na yote haya yataimarisha ushawishi wa China.
Wakati huo huo, ili kumridhisha Urusi na kupata msaada wa watu wake, nchi hizi ziliharakisha kutoa taarifa dhidi ya Marekani na Uingereza.
Hitimisho:
Shirika la Ushirikiano la Shanghai limeanza kubadilika hatua kwa hatua kuwa shirika linalohudumia maslahi ya kiuchumi na kiusalama ya China zaidi ya malengo ambayo liliundwa kwa ajili yake mwanzoni. Suala la utulivu wa kikanda limesalia kuwa kauli mbiu tu kwenye karatasi. Hili linathibitishwa na misimamo ya shirika kuelekea idadi ya mizozo ya kijeshi. Kwa mfano, wakati mzozo wa silaha ulizuka kati ya India na Pakistan, ambazo ni wanachama wa shirika, shirika halikuchukua hatua yoyote, wala halikutoa msimamo rasmi. Vile vile, katika msimu wa vuli wa 2022, wakati mzozo wa mpaka ulizuka kati ya Tajikistan na Kyrgyzstan wakati wa mkutano wa shirika huko Samarkand.
Kwa hiyo, Shirika la Ushirikiano la Shanghai na mifano kama hiyo si chochote ila mtego wa kikoloni uliowekwa kwa Waislamu. Waislamu hawataokoka kutoka kwa makucha haya ya kikoloni isipokuwa kwa kurudi kwenye Uislamu wao. Hili ndilo ambalo makafiri wakoloni na watawala wetu vibaraka wanajua vizuri, na kwa hivyo wanatupiga vita kwa kisingizio cha kupambana na "ugaidi, itikadi kali na kujitenga".
Imeandikwa na: Profesa Mumtaz Ma Wara Al-Nahri
Chanzo: Gazeti la Ar-Raya