Hotuba ya Erdogan katika Umoja wa Mataifa: Maneno Matupu!
(Imetafsiriwa)
Habari:
Katika hotuba yake kwa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Erdogan alielezea kile kinachotokea Gaza kama mauaji ya kimbari, akisisitiza kwamba taasisi ya Kiyahudi inaua watoto kila siku, na akatoa wito kwa mfumo wa kimataifa kuchukua hatua. Alichapisha picha kutoka Gaza, na kusema: "Hakuna vita huko Gaza; ni sera ya uvamizi, uhamishaji na mauaji ya halaiki."
Alirudia msemo wake maarufu "Ulimwengu ni mkuu kuliko tano," akikosoa muundo wa Umoja wa Mataifa, na akatangaza kwamba uhusiano na Shirika la Mkataba wa Atlantiki ya Kaskazini (NATO) na Amerika unaimarika, na kwamba Uturuki itakuwa mwenyeji wa mkutano wa kilele wa shirika hilo mwaka 2026. Miongoni mwa mambo muhimu mengine katika hotuba yake ni umakini wake kuhusu mazingira, akili bandia, kupunguza taka na familia.
Maoni:
Erdogan alielekeza umakini kwa masuala mengi ya kimataifa, hasa suala la Palestina. Hata hivyo, maneno yake, kwa mtazamo wa Kiislamu, yanaonekana kuwa matupu, yamejitenga na uhalisia, hayako huru na vizuizi vya mfumo wa kikoloni wa kimataifa.
Huenda maneno ya Erdogan yamegusa hisia, hasa kuhusu Palestina. Lakini kwa mtazamo wa Kiislamu, kasoro kubwa katika hotuba hii ni kwamba maneno hayo yenye nguvu hayatafsiriwi kuwa matendo. Wakati watoto wa Gaza wanakufa kwa njaa, na eneo hilo linageuka kuwa kambi ya kifo na uharibifu chini ya mzingiro kamili, sauti ya wanaodhulumiwa ni maneno tu.
Ukosoaji wake kwa Umoja wa Mataifa pia ulikuwa wa juu juu. Umoja wa Mataifa ambao unaitwa "kurekebishwa" ni mfumo uleule ulioanzishwa na wadhalimu. Wajibu wa umma si kuuhuisha, bali kuanzisha mfumo mpya wa kimataifa kwa misingi ya Uislamu. Inaonekana kwamba msemo wa Erdogan unaorudiwa "Ulimwengu ni mkuu kuliko tano" ni ukosoaji wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye wanachama watano. Ingawa msemo huu umepokea mwangwi mzuri miongoni mwa watu wanaodharau mfumo wa kimataifa, ukweli ni kwamba Amerika yenyewe haifurahishwi na mfumo wa baada ya Vita vya Pili vya Dunia iliyounda na inataka kuubadilisha. Kwa hivyo, wito wa Erdogan wa mageuzi unaambatana na maslahi ya Amerika yenyewe.
Zaidi ya hayo, sifa ya Erdogan ya kuimarisha uhusiano na NATO ni udhalilishaji kwa Waislamu, si heshima kwao. Ushirikiano na shirika ambalo limeua mamilioni ya Waislamu kutoka Afghanistan hadi Iraq, na kutoka Syria hadi Libya, si jambo la kujivunia, bali ni jambo la aibu.
Pia, dhana ya "suluhisho la mataifa mawili" ni zao la mawazo ya kikoloni. Katika muktadha wa Palestina na Cyprus, msemo huu unamaanisha tu kutambua uwepo wa Wayahudi kwenye ardhi ya Palestina na uwepo wa Wagiriki katika kisiwa cha Cyprus. Hata hivyo, wote wawili wamevamiwa. Suluhisho si kuhalalisha uvamizi huu na kuutambua, bali kuukomesha.
Ingawa hotuba ya Erdogan ilijumuisha maneno na maoni ya kushangaza, haina uzito wowote ikilinganishwa na msimamo halisi wa kisiasa wa Uturuki katika miaka miwili iliyopita katikati ya mauaji ya kimbari yanayoendelea huko Gaza.
Maelezo ya mkutano wa Erdogan na Trump baada ya hotuba yake katika Umoja wa Mataifa yanaonyesha jinsi Uturuki, licha ya eneo lake kubwa la kimkakati na mienendo ya nguvu kubwa, imeanguka katika hali ya udhaifu. Makubaliano makubwa yalifikiwa na Amerika ambayo wigo wake kamili bado haujafichuliwa. Miongoni mwa vipengele vyake ni ujenzi wa mitambo ya nyuklia ya kiraia nchini Uturuki, ununuzi wa Shirika la Ndege la Uturuki wa mamia ya ndege za abiria kutoka Amerika, ndege za kivita za aina ya F-35 na F-16, vifaa vya kijeshi, usafirishaji wa gesi asilia iliyoyeyushwa kupitia meli za Amerika, na hata ugawaji wa baadhi ya madini adimu ya ardhini kutoka Uturuki kwenda Amerika.
Kukaribishwa kwa Trump kwa Erdogan alipoingia, matumizi yake ya itifaki ya ngazi ya juu, kuvuta kiti chake, kuketi karibu naye, kufanya mkutano wa faragha wa zaidi ya saa mbili, na kumsifu mara kwa mara, haikuwa bila sababu.
Maneno ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio yanaeleza ambapo alisema: "Mataifa mengine yote, ikiwa ni pamoja na Uturuki, kimsingi yanatuomba tuingilie kati katika masuala haya... Hatimaye, kuna viongozi ambao wanaomba kushiriki katika hili. Wanapiga simu na kusema: Je, tunaweza kusalimiana na Rais kwa dakika tano?".
Wakati viongozi wengi wa ulimwengu wanaomba kusalimiana na Trump kwa dakika tano, mkutano wa Erdogan wa saa mbili unaonyesha makubaliano makubwa yaliyotolewa na Uturuki na majukumu mapya ambayo imepangwa kuchukua katika utekelezaji wa mipango ya kikanda ya Amerika!
Imeandikwa kwa Idhaa ya Afisi ya Habari Kuu ya Hizb ut-Tahrir
Ramzi Uzair