Jinsi Watawala wa Kiislamu Walivyoitelekeza Gaza kwa Ajili ya Diplomasia na Mikataba!
(Imetafsiriwa)
Habari:
Rais wa Indonesia Prabowo Subianto ametoa wito wa kusitishwa mara moja kwa mapigano kati ya chombo cha Kiyahudi na Hamas, na kupunguza mivutano kati ya chombo hicho na Iran. Wakati wa mkutano wake na Waziri Mkuu wa Singapore Lawrence Wong, Prabowo alisisitiza umuhimu wa suluhisho la amani kupitia diplomasia. Alielezea wasiwasi wake mkubwa juu ya vifo vya watu huko Gaza na kuongezeka kwa mvutano katika Mashariki ya Kati. Pia aligusia mgogoro wa Myanmar, akisisitiza dhamira ya ASEAN ya kutekeleza makubaliano ya vipengele vitano ili kukomesha ghasia na kukuza mazungumzo jumuishi. Indonesia na Singapore zimehakikisha makubaliano yao ya kuendelea kuunga mkono ushiriki wa amani nchini Myanmar, na kuimarisha utulivu wa kikanda na juhudi za misaada ya kibinadamu. (Chanzo)
Maoni:
Tangu kuzuka kwa vita dhidi ya Gaza mwaka 2023, serikali ya Indonesia imeshughulikia suala la Palestina kama hotuba ya kisiasa tu, bila hatua yoyote ya kweli na madhubuti. Hata mahusiano ya kibiashara kati ya Indonesia na chombo cha Kiyahudi yameendelea bila kukatizwa.
Msimamo huu unafanana na majibu ya idadi ya watawala wa Kiislamu wa Kiarabu ambao wanajifanya kuwa wanajali suala la Palestina na wanatoa shutuma za wazi dhidi ya vitendo vya Kizayuni, lakini hawachukui hatua zozote za dhati za kukomesha mauaji dhidi ya ndugu zao Waislamu huko Palestina.
Kinachosikitisha zaidi ni kwamba watawala hawa wameonyesha ukaribu unaoongezeka na Marekani, ambapo walimkaribisha Rais wa Marekani Trump kwa mapokezi makubwa mwezi Mei 2025, na kutangaza ahadi za uwekezaji mkubwa. Hili ni jambo linalotia wasiwasi sana, kwa sababu Marekani ndiyo mfuasi mkuu wa chombo cha Kiyahudi, na inahakikisha kuwa inakiuzia silaha zinazotumiwa kuwachinja raia huko Gaza.
Iran iliposhambuliwa na chombo cha Kiyahudi, nchi za Kiislamu jirani zilibaki katika msimamo wa mtazamaji. Hata baadhi yao walishiriki, katika baadhi ya matukio, katika juhudi za kuzuia makombora ya Iran kwa kushirikiana na majeshi ya Kizayuni na Marekani.
Jibu la Iran lilipaswa kuwa cheche ya kuchochea mshikamano mpana wa Kiislamu ili kudhoofisha muungano wa chombo cha Kiyahudi na Marekani. Lakini, kwa bahati mbaya, fursa hii ilipotea kwa sababu ya upofu wa serikali hizi kwa ukweli.
Mpaka sura ya kisiasa ya kilimwengu ya nchi za Kiislamu ibadilike kuelekea mbinu halisi ya Kiislamu, hakutakuwa na matumaini makubwa ya kuchukua hatua za kweli za kuwatetea watu wa Palestina au kuwalinda Waislamu ulimwenguni kote.
Imeandikwa kwa ajili ya Radio ya Afisi ya Habari Kuu ya Hizb ut-Tahrir
Abdullah Aswar