Pamoja na Hadithi Tukufu
Ufahamu wa Dini Ni Bora Duniani na Bora Akhera
Tunawasalimu nyote wapenzi wetu popote mlipo, katika kipindi kipya cha programu yenu "Pamoja na Hadithi Tukufu" na tunaanza na salamu bora, Assalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh.
Kutoka kwa Muawiya, alisema: Nilimsikia Mtume, swallallahu alayhi wasallam, akisema: «Yeyote ambaye Mwenyezi Mungu anamtakia kheri, humfanya aelewe dini». Imesimuliwa na Bukhari namba 71.
Enyi wasikilizaji wetu waheshimiwa:
Ufahamu wa dini umekuwa nguzo kuu katika ulimwengu wa Uislamu na Waislamu kwa karne nyingi. Waislamu wamekuwa na jukumu muhimu katika historia ya Uislamu tangu Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunnah za Mtume wake, swallallahu alayhi wasallam, vilipokuwa kitovu cha umakini katika maisha yao. Jambo hilo lilikuwa kubwa kwao na halikuwa la mzaha. Vipi isiwe hivyo wakati waligundua kuwa kheri yote iko katika ufahamu na uandishi? Urithi huu mkuu wa vitabu walioacha ulitokana na ufahamu wao wa umuhimu wa fiqhi na umuhimu wa Uislamu kuwa mstari wa mbele, na kwamba Uislamu unashinda na haushindwi.
Enyi Waislamu:
Hali imebadilika baada ya kubomolewa kwa dola ya Ukhalifa, na nguvu za Waislamu zikageuka kuwa udhaifu, na heshima yao kuwa hofu. Kalamu zikaanza kuandika fiqhi mpya kwa wino wa kibepari, na kwa mikono ya kilimwengu, na fiqhi ikawa ngeni kwa umma huu. Sauti za utaifa na uzalendo zikainuliwa ndani yake, na watu wakaitana kwa ushabiki na ukanda, na umma ukatengana, kila mmoja akiimba wimbo wake, hakuna mtawala anayezuia, wala dola inayokusanya, watu duni wa uumbaji wanautesa umma. Ndio, hivi ndivyo fiqhi ilivyodhoofika katika nafsi na akili kwa miaka mingi. Leo, baada ya umma kurejea katika akili zake, na kuanza kutafuta fiqhi yake, umetambua kuwa Uislamu ndio uliotengeneza historia yake, viongozi wake, na watu wake ambao walieneza Uislamu katika sehemu zote za dunia, na kuijaza fiqhi, uadilifu, fikra, na elimu. Kwa hivyo, ufahamu wa dini ni bora duniani na bora akhera.
Ewe Mwenyezi Mungu, tuharakishie Ukhalifa ulioongoka kwenye njia ya Utume ambao utakusanya yaliyotawanyika ya Waislamu, uwaondoe katika balaa walilomo. Ewe Mwenyezi Mungu, nurisha ardhi kwa nuru ya uso wako mtukufu. Ewe Mwenyezi Mungu, Amin, Amin.
Wapenzi wetu waheshimiwa, na hadi tutakapokutana nanyi na hadithi nyingine ya kinabii, tunawaacha katika uangalizi wa Mwenyezi Mungu, na Assalamu Alaikum Warahmatullahi Wabarakatuh.
Imeandikwa kwa ajili ya redio na: Abu Maryam