Kukataliwa kwa Wanariadha kutoka Utawala wa Kiyahudi: Je, Hii ni Mtihani Halisi wa Msimamo Thabiti wa Indonesia?
Habari:
Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo imekataa rufaa za Shirikisho la Utawala wa Kiyahudi la Gymnastics kuhusu ushiriki wa wanariadha wake katika Mashindano ya Dunia ya Gymnastics ya Sanaa huko Jakarta, Indonesia, kutoka Oktoba 19 hadi 25, 2025. Serikali ya Indonesia ilikataa kutoa visa vya kuingia kwa wanariadha sita kutoka Utawala wa Kiyahudi, ikiunga mkono Palestina na kujibu shinikizo la ndani. Shirikisho la Utawala wa Kiyahudi la Gymnastics liliwasilisha rufaa kwa Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo na Shirikisho la Kimataifa la Gymnastics ili kuhakikisha ushiriki au kufuta mashindano hayo. Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo ilikataa rufaa hizo, na Shirikisho la Kimataifa la Gymnastics lilisema kuwa halina mamlaka juu ya maamuzi ya visa. Indonesia ilisisitiza msimamo wake kwa mujibu wa sera yake ya kigeni na maoni ya umma ya ndani. (en.antaranews.com)
Maoni:
Uamuzi wa Indonesia kukataa ushiriki wa wanariadha kutoka Utawala wa Kiyahudi katika Mashindano ya Dunia ya Gymnastics ni hatua ya kupongezwa, kwani inaonyesha msimamo thabiti wa Indonesia dhidi ya Utawala wa Kiyahudi. Hatua hii inapaswa kuchukuliwa kama mwanzo wa kuchukua msimamo thabiti na endelevu dhidi ya uwepo wa Utawala wa Kiyahudi nchini Indonesia, sio tu katika uwanja wa michezo, bali pia katika nyanja za uchumi, utalii, elimu na zinginezo.
Licha ya kwamba Indonesia imekuwa ikisisitiza uungaji mkono wake thabiti kwa uhuru wa Palestina na haijaanzisha uhusiano rasmi wa kidiplomasia na Utawala wa Kiyahudi, uhusiano usio rasmi bado upo. Katika miaka ya hivi karibuni, idadi ya wanariadha wa Utawala wa Kiyahudi wameshiriki katika mashindano yaliyofanyika Indonesia, akiwemo Misha Zilberman, mchezaji wa badminton ambaye alishiriki katika Mashindano ya Dunia ya 2015 huko Jakarta, Yuval Shemla, mpanda milima ambaye alishiriki katika Kombe la Dunia la Kupanda Milima la 2022 huko Jakarta, na Mikhail Yakovlev, mwendesha baiskeli ambaye alishinda medali ya shaba katika Kombe la Mataifa la Baiskeli la 2023. Pia, ujumbe kutoka bunge la Utawala wa Kiyahudi ulihudhuria mkutano wa 144 wa Umoja wa Mabunge Duniani huko Bali mwaka 2022, ingawa haukualikwa rasmi na Indonesia.
Kwa upande wa kibiashara, shughuli za kibiashara kati ya Indonesia na Utawala wa Kiyahudi zinaendelea kupitia wahusika wengine kama vile Singapore na Hong Kong. Mnamo 2024, uagizaji wa bidhaa za Indonesia kutoka Utawala wa Kiyahudi ulifikia karibu dola milioni 54.2 za Kimarekani, na ulijumuisha mashine za kimitambo, vifaa vya umeme, bidhaa za macho na dawa. Wakati mauzo ya Indonesia kwa Utawala wa Kiyahudi yalifikia karibu dola milioni 236, na muhimu zaidi yalikuwa viatu vya ngozi, mafuta ya mawese na bidhaa za nguo. Vile vile, katika sekta ya utalii, maelfu ya watu kutoka Utawala wa Kiyahudi waliruhusiwa kutembelea Indonesia, na Waindonesia wengi husafiri kwenda huko.
Takwimu hizi zinaonyesha kuwa msimamo wa Indonesia dhidi ya Utawala wa Kiyahudi haujakuwa thabiti kabisa. Kwa hivyo, kukataliwa kwa wanariadha wake hivi karibuni kunapaswa kuwa hatua ya kwanza kuelekea sera endelevu na kamili dhidi yake katika nyanja zote. Hata hivyo, ikiwa uamuzi huu hautaambatana na misimamo kama hiyo katika nyanja zingine, basi hiyo inazua swali muhimu: Je, uamuzi huo ulichochewa na mshikamano wa kweli na Palestina, au ulitokana tu na kujibu shinikizo la maoni ya umma kukataa uwepo wa Utawala wa Kiyahudi nchini Indonesia?
Itakuwa bahati mbaya ikiwa sababu ni shinikizo la umma tu, kwa sababu hiyo itamaanisha kuwa msimamo wa Indonesia kuelekea Palestina hauna umakini, na kwamba Indonesia haitofautiani na nchi zingine zinazounga mkono Palestina kwa maneno huku zikiwa na uhusiano na Utawala wa Kiyahudi.
Msimamo huu unapaswa kuwa wito wa kutafakari kwa watu wa Indonesia, kuendelea kushinikiza serikali kwa ajili ya kuwepo kwa uwiano kati ya maneno na matendo. Pia, unapaswa kuwa somo kwa nchi zote za Kiislamu kwamba mradi tu tawala zilizopo humo zinakamatwa na maslahi finyu ya kitaifa, masuala ya kibinadamu na masuala ya umma wa Kiislamu yataendelea kuwekwa pembeni. Kwa hivyo, Waislamu hawapaswi kuishia na mapambano yao kwa masuala ya muda mfupi, bali wajitahidi kuanzisha utawala wa Kiislamu ambao unazingatia kweli maslahi yao ulimwenguni kote.
Imeandikwa kwa Idhaa ya Ofisi Kuu ya Habari ya Hizb ut-Tahrir
Abdullah Aswar